arehe 28 Mei 2026 Mhe.Balozi Agnes Richard Kayola alikutana na kufanya mazungumzo na Bw.Evance Lundo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Safe Equipment and General Supplies. Kampuni hiyo yenye makao makuu jijini Dar es Salaam, Tanzania inajihusisha na uagizaji na usambazaji wa vifaa tiba ndani na nje ya nchi. Vifaa hivyo ni pamoja na Vifaa vya Mazoezi tiba (Physiotherapy), Upasuaji mifupa (Orthopaedic), Vifaa vya joto kwa watoto wachanga (baby incubators), vifaa vya maabara na vitanda vya kujifungulia kinamama. Lengo la mazungumzo hayo lilikua ni kujadiliana na kuhusu fursa za soko la vifaa tiba nchini Malawi. Katika majadiliano hayo, Ndugu Evans alibainisha kuwa Kampuni yake imesajiliwa na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA) na inashirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania ikiwemo kuwa na mkataba wa usambazaji vifaa tiba na Bohari Kuu ya Dawa na tayari wamefanya kazi na baadhi ya hospitali ikiwemo hospitali ya Taifa Muhimbili.
Kwa upande wake Mhe.Balozi Kayola alimpongeza Bw. Evance kwa jitihada zake za kutafuta soko la bidhaa zake nchini Malawi. Aidha, alimfahamisha kuwa pamoja na changamoto za kiuchumi zinazoikabili Malawi ikiwemo kushuka kwa thamani ya Kwacha na uhaba wa fedha za kigeni hususan Dola za Marekani bado fursa za soko la vifaa tiba lipo. Vilevile, Mhe. Balozi alimkaribisha Dkt. Rajab ambaye ni Mtanzania anayefanya kazi zake nchini Malawi ili atoe uzoefu wake kuhusu fursa zilizopo nchini Malawi katika soko la vifaa tiba. Kwa uzoefu wake Dkt. Rajab alieleza kuwa soko la vifaa tiba nchini Malawi lipo kwa baadhi ya maeneo ikiwemo mashine za kusafisha damu kwa wagonjwa wa figo (Dialysis), Mifuko ya kuhifadhia damu salama, gozi ambazo zinatumika zaidi ya mara moja (re-usable) na anti cancer drugs. Aidha, Dkt.Rajab alimfahamisha Ndugu Evance kuwa atampatia ushirikiano katika kupata fursa za masoko ya vifaa tiba kwa kuwa naye ana uzoefu na anajihusisha na masuala hayo. Vilevile, alimuahidi kumpatia taarifa kuhusu zabuni za vifaa tiba zitakazotolewa ili aweze kuona anazoweza kuzifanyia kazi. Mhe. Balozi alihitimisha kwa kumtakia kila la kheri Bw. Evance na kumshukuru Dkt. Rajab kwa kutoa ushirikiano kuhusu uzoefu wake katika masuala ya afya hususan fursa zilizopo Malawi za vifaa tiba.



